Tarehe 24 na 25 Mei, 2025, mji mkuu wa Kepuvede (Cape Verde), Praia, uliandaa tukio la kihistoria: Jukwaa la Kwanza la Kepuvede kuhusu Uhuru wa Kidini (FELIR 2025). Tukio hili liliandaliwa na Idara ya Uhuru wa Kidini na Masuala ya Umma ya Chama cha Makanisa ya Waadventista wa Sabato nchini Kepuvede (AIASD-CV), na lilifanyika katika Ukumbi wa Heshima wa Bunge la Kitaifa, kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru wa taifa na miaka 90 tangu kuwasili kwa Kanisa la Waadventista wa Sabato nchini humo.
Kukuza Mazungumzo na Kulinda Haki
Muundo wa kidini wa Kepuvede unatawaliwa na Ukristo. Kwa mujibu wa takwimu za hivi karibuni za kitaifa za mwaka 2021, asilimia 72.5 ya wakazi wenye umri wa miaka 15 na zaidi wanajitambulisha kama Wakatoliki, wakifuatiwa na Waadventista wa Sabato ambao ni asilimia 1.9.

Washiriki walisema kuwa tukio hili lilijitokeza kwa tabia yake ya wingi wa mitazamo na kutokuwa na upendeleo wa kidini, na kwa kutoa nafasi ya mazungumzo ya wazi na jumuishi. Tukio hili liliwakaribisha viongozi wa serikali, wataalamu wa sheria, wawakilishi wa asasi za kiraia, wataalamu wa kitaifa na kimataifa, na mashirika yanayojitolea kukuza haki za kibinadamu. Zaidi ya watu 600 walihudhuria ana kwa ana, huku wengi zaidi wakifuatilia mtandaoni.
Kukuza Mazungumzo na Kulinda Haki
Sherehe ya ufunguzi tarehe 24 Mei ilihudhuriwa na Rais wa Jamhuri, Dkt. José Maria Neves, ambaye alithibitisha tena ahadi ya Kepuvede kwa amani na uvumilivu wa kidini, akisisitiza umuhimu wa kutatua haraka vikwazo vyovyote vya kisheria vinavyoathiri utekelezaji wa uhuru huu.
Watoa mada walijadili mada kuu kutoka mitazamo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na dhamana za kikatiba, uhusiano kati ya dini na siasa nchini Kepuvede, na mafanikio na changamoto zinazohusiana na uhuru wa kidini, hasa ushiriki wa Waadventista wa Sabato katika mitihani ya umma na sehemu za kazi.
Miongoni mwa watoa mada mashuhuri wa jukwaa walikuwa Dkt. Aristides Lima, mmoja wa majaji watatu wa Mahakama ya Katiba (mahakama kuu ya Kepuvede); Dkt. Adilson Semedo, mtafiti katika Chuo Kikuu cha Kepuvede; Dkt. Eurídice Mascarenhas, mwenyekiti wa Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu na Uraia; na Dkt. Felisberto Moreira, mwenyekiti wa Mtandao wa Kitaifa wa Haki za Kibinadamu.
Wageni wa kimataifa walikuwa pamoja na wakili wa Waadventista Dkt. Damaris Moura, mwandishi wa sheria ya kwanza ya Brazili kuhusu uhuru wa kidini, na Dkt. Fábio Nascimento, rais wa Muungano wa Nchi Zinazozungumza Kireno kwa ajili ya Uhuru wa Kidini.

Hadithi ya Uvumilivu na Matumaini
Wakati wa tukio hilo, António Monteiro dos Anjos, mchungaji wa Waadventista kutoka Kepuvede, alishiriki uzoefu wake wa kufungwa nchini Togo. Mwaka 2012, alikamatwa kwa tuhuma zisizo na msingi za kuhusika na mtandao wa usafirishaji haramu wa binadamu. Licha ya ukosefu wa ushahidi, alikaa gerezani mjini Lomé kwa miezi 22. Katika kipindi hicho, Kanisa la Waadevntista duniani liliungana kumtetea kupitia maombi, kampeni za mitandaoni, na ombi la kimataifa. Tarehe 13 Januari, 2014, Mahakama ya Rufaa ya Togo ilimtangaza kuwa hana hatia na kuamuru aachiliwe.
Kesi ya Monteiro iligeuka kuwa mfano wa utetezi wa uhuru wa kidini na haki za kibinadamu, ikionyesha hatari zinazowakabili viongozi wa kidini katika mazingira ya kutovumiliana na ukosefu wa haki. Ushuhuda wake katika jukwaa uliimarisha umuhimu wa kulinda uhuru wa kidini na haki za kimsingi katika kila jamii.
Ahadi ya Waadentista kwa Uhuru
Katika hotuba yake ya ufunguzi, Natalino Martins, rais wa Kanisa la Waadventista nchini Kepuvede, alisisitiza kuwa uhuru wa kidini ni haki ya asili na isiyoweza kutengwa, inayotokana na Biblia kupitia zawadi ya Mungu ya hiari ya kuchagua, inayomruhusu mtu kuchagua imani yake bila kulazimishwa. Alitaja mchango wa kihistoria wa Kanisa la Waadventista katika kutetea haki hii, ikiwa ni pamoja na mchango wa Ellen G. White na Mchungaji Alonzo T. Jones, mmoja wa waanzilishi wa Chama cha Kimataifa cha Uhuru wa Kidini (IRLA), shirika kongwe zaidi duniani linalojishughulisha na uhuru wa kidini pekee.
Alitoa shukrani kwa Serikali ya Kepuvede, inayowakilishwa na Rais wa Jamhuri, pamoja na Katiba na Sheria Na. 64/VIII/2014, inayoweka msingi wa kisheria wa uhuru wa kidini na ibada. Alisisitiza Kifungu cha 49 cha Katiba, kinachohakikisha heshima kwa uhuru wa kidini. Hata hivyo, alitaja changamoto zilizopo, ikiwa ni pamoja na ukosefu wa utaratibu kwa Waadventista wasioweza kushiriki mitihani siku ya Jumamosi.

“Nathibitisha tena dhamira yetu ya kuendelea kufanya kazi bega kwa bega na Serikali, jumuiya nyingine za kidini, na jamii ya kiraia,” alisema Martins, “ili uhuru wa kidini usiwe tu sheria iliyoandikwa na Mungu na wanadamu, bali uwe uhalisia unaoishi—uliojaa heshima na imani.”
Kuangalia Mbele
Mwisho wa jukwaa hilo, David Njock, rais wa Misheni ya Yunioni ya Sahel Magharibi ya Waadventista wa Sabato (UMOS), alitoa wito wa “mtazamo wa neema zaidi ya tofauti zetu za kidini,” akisisitiza thamani ya utofauti kama fursa ya kukua pamoja. Hata hivyo, alifafanua kuwa uvumilivu wa kidini haupaswi kuchanganywa na kukubali vitendo vinavyokiuka utu wa binadamu.
Kwa mujibu wa Profesa Milton Monteiro, mjumbe wa Cape Verde katika kamati ya maandalizi na mwanzilishi wa Chama cha Uhuru wa Kidini cha Kepuvede (ACLIR), “Tukio hili ni hatua ya kihistoria nchini Kepuvede na linathibitisha tena ahadi ya Waadventista wa Sabato kwa utu wa binadamu, haki za kibinadamu, na uhuru wa kidini.”
Inatarajiwa kuwa kutakuwa na utiaji saini rasmi wa “Tamko la Praia kuhusu Uhuru wa Dini” katika hafla ijayo, pamoja na ushirikiano na mikataba inayolenga kuimarisha ushirikiano kati ya mashirika ya kidini, taasisi na Serikali. Mawakili na wasomi Waadventista pia walipendekeza muswada wa kuanzisha Siku ya Kitaifa ya Uhuru wa Kidini. Tovuti rasmi ilizinduliwa wakati wa tukio hilo.
Makala asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Kireno ya Divisheni ya Amerika Kusini. Jiunge na Chaneli ya WhatsApp ya ANN kwa habari za hivi punde za Waadventista.