Mnamo Julai 5, 2025, Kanisa la Waadventista Wasabato Amerika Kaskazini (NAD) liliwasilisha ripoti ya kwanza ya divisheni katika Kikao cha Konferensi Kuu (GC) cha 2025.
Rais wa NAD, G. Alexander Bryant, katibu Kyoshin Ahn, na mhasibu Judy R. Glass waliwasilisha video iliyolenga shughuli na mafanikio ya huduma ya divisheni hiyo katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita. Ingawa muda wa ripoti hii ulipunguzwa kutokana na janga la kidunia, athari ya divisheni katika miaka hii imekuwa ya kina na yenye umuhimu mkubwa.
Gerson P. Santos, katibu msaidizi wa GC, aliitambulisha divisheni yake ya “kulea,” akieleza kuwa NAD ndiyo divisheni kubwa zaidi kijiografia, ikienea katika nchi na maeneo tisa na kanda za saa 14, ikiwa na washiriki zaidi ya 1.3 milioni katika karibu makutaniko 7,000, wakisali kwa zaidi ya lugha 30. Eneo lake pia linajumuisha takribani shule 1,000, vyuo vikuu na taasisi 13 za elimu ya juu, mtandao mkubwa wa hospitali na kliniki, pamoja na huduma kadhaa za vyombo vya habari.
Katika maneno yake ya utangulizi kabla ya video kuchezwa, Bryant alisema: "Kuna methali ya Kiafrika inayosema, ukitaka kwenda haraka, nenda peke yako, lakini ukitaka kufika mbali, nendeni pamoja. Kauli mbiu ya Divisheni ya Amerika Kaskazini kwa miaka mitatu iliyopita imekuwa Pamoja katika Misheni. Inajengwa juu ya imani kwamba tunakuwa na nguvu zaidi tukiwa pamoja na tunaweza kufanya athari kubwa zaidi kwa ajili ya Kristo tunapofanya kazi kwa pamoja; na tunapounganishwa pamoja, bega kwa bega na moyo kwa moyo — kanisa la eneo, shule za eneo, taasisi za afya na elimu ya juu, konferensi za eneo, yunioni, divisheni, Konferensi Kuu — tukitumia rasilimali na mali zetu kwa njia ya umoja ili kuendeleza misheni ya Mungu, tunakuwa nguvu isiyoshindika.”
Bryant alitaja maeneo matatu ya kimkakati ya NAD, au M tatu: kuzidisha, vyombo vya habari, na ulezi, yaani (three Ms: multiply, media, and mentorship).
“Kuzidisha... kunahusu jinsi tunavyoweza kuzidisha huduma ya Yesu kwa ufanisi zaidi. Haimaanishi kwamba hatujawahi kufanya huduma za Yesu. Lakini tunawezaje kuzifanya kwa ufanisi zaidi, kwa athari kubwa zaidi? Huduma ya kufundisha ya Yesu, huduma ya uponyaji ya Yesu, huduma ya kutangaza ya Yesu, huduma ya huruma ya Yesu, vyote vikija pamoja kwa athari moja.”
Aliendelea, “Pentekoste 2025 ni mfano wa mtazamo huu, ambapo [ngazi zote za kanisa zinaungana] kusonga mbele na mpango huu kote katika eneo la Divisheni ya Amerika Kaskazini. Hii ndiyo kuzidisha: kuzidisha huduma za Kristo, kuzidisha athari za Kristo, na kuzidisha ushawishi wa huduma ya Yesu.”
Kisha alimgeukia Glass, ambaye alizungumza kuhusu vyombo vya habari (Media), M ya pili.
“Kwa kutumia nguvu ya vyombo vya habari, washiriki wa kanisa la Amerika Kaskazini wanaunganishwa na watu wanaotafuta kumjua Mungu zaidi, na kisha kuwasaidia kupata jamii ya imani,” alisema Glass.
Alishiriki kwamba “wanafunzi wa kidigitali zaidi ya 13,000 wamefundishwa katika mpango unaoendelea wa kuwafundisha washiriki jinsi ya kushiriki imani yao kupitia mazungumzo ya moja kwa moja.”
Glass alisisitiza kwamba kupitia huduma ya mazungumzo ya moja kwa moja kwenye Adventist.org, “maswali kuhusu imani yanajibiwa, maombi ya sala yanapokelewa, na watu wanaunganishwa na makanisa ya karibu.”
Alibainisha kuwa huduma zinazowalenga watu moja kwa moja kama Faith for Today pia zinatumia nguvu ya vyombo vya habari vya matangazo kushiriki neema ya Mungu.
Alimalizia kwa kusema, “Miunganisho hii ya kidigitali inafungua milango ya kujenga urafiki na kushiriki upendo wa Mungu.”
Hatimaye, Ahn alitoa muhtasari wa M ya tatu — ulezi(mentorship) — kabla ya ripoti ya video ya divisheni kuonyeshwa kwa maelfu waliohudhuria Kikao cha Konferensi Kuu na waliokuwa wakitazama mubashara.
“Tunaamini ulezi ni sehemu muhimu ya misheni wetu. Ulezi unamaanisha kutembea pamoja na wengine, kushiriki hekima, kutoa moyo, kusikiliza hadithi zao, na kuwawezesha wengine na vizazi vijavyo kutumika kwa ujasiri na huruma ili kutimiza misheni ya kanisa katika dunia hii,” alisema, akiendelea, “Umejengwa juu ya Maandiko, maombi na ahadi ya pamoja kwa Kristo. Kupitia mchakato huu wa kulea, imani inakuzwa, viongozi wanaandaliwa, na kanisa la ndani linakuwa imara.”
Ahn alihitimisha utangulizi wa viongozi wa NAD kwa maono yanayotia moyo: “Tunaona kanisa ambapo viongozi waliokomaa wanawalea vijana, na ambapo wachungaji wenye uzoefu wanainua sauti zinazochipuka, ili kila mshiriki, kila muumini katika eneo letu, awe analelewa na pia analea wengine, yote kwa ajili ya Kristo. Ndugu na dada, hii hapa ripoti ya Divisheni ya Amerika Kaskazini. Asanteni.”
Mambo Muhimu Kutoka Ripoti hiyo ya NAD
Hapa chini kuna mambo muhimu kutoka ripoti hiyo ya Divisheni ya Amerika Kaskazini.
Tangu mwaka 2022, washiriki na viongozi wa NAD kote Bermuda, Kanada, Guam-Mikronesia, na Marekani wameungana kwa majibu yao binafsi na ya pamoja kwa wito wa Kristo wa kufanya wanafunzi, wakitekeleza mpango wa kimkakati wa Kanisa la Waadventista wa Sabato duniani: “Nitakwenda.”
Chini ya kaulimbiu ya miaka mitano, “Pamoja katika Misheni,” ikiwa na vipaumbele vitatu vya kuzidisha wanafunzi, kutumia vyombo vya habari kwa ajili ya kufikia watu, na kulea viongozi wa sasa na wa kizazi kijacho, divisheni imepiga hatua katika kusambaza ujumbe wa kipekee wa Waadventista wa Sabato unaomweka Kristo katikati, wa matumaini na uzima kamili katika eneo lake. Tangu mwaka 2022, familia ya NAD imepokea washiriki wapya 204,357 katika makanisa 6,810 na makampuni 894.
Hadithi ya jinsi Kanisa la Waadventista wa Sabato katika Amerika Kaskazini limeendelea kukua katika mazingira magumu baada ya COVID-19 ina sura nyingi na ni tata; hivyo, iliwasilishwa kwa hadhira ya Kikao cha Konferensi Kuu kwa kuigawa katika sura tano.
Sura ya 1: Kuzidisha Wanafunzi
Katika Amerika Kaskazini, ufuasi wa Kristo mara nyingi huanza na mbegu — neno la upole, wakati wa kuunganishwa, tendo la huduma — inayopandwa katika nyumba, shule, migahawa, na ibada za mtandaoni. Kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, mbegu hizi hukua na kuwa vituo vya ushawishi, vikundi vidogo, na makutaniko mapya.
Kama moja ya vituo vya ushawishi vinavyokua vya NAD, Kituo cha Urban Life cha Konferensi ya Chesapeake kilichopo Baltimore, Maryland, kinafikia jamii yake kupitia programu za afya, matukio ya kijamii, na huduma zinazolenga mahitaji ya watu. Kikiwa ni matokeo ya ushirikiano wa kimkakati kati ya makanisa mawili ya eneo hilo, kituo hiki kinalenga kuwa daraja kati ya mahitaji ya jamii na ujumbe wa injili. Katika ripoti ya video, mkurugenzi wake, Cristina Macena, alieleza kwamba kituo hiki “ni mahali ambapo watu wanapata tumaini, kusudi, na uponyaji. Sio ukuaji tu — ni mabadiliko.”
Kwa kuzingatia mbinu ya Kristo ya kuchangamana na watu, kutambua na kukidhi mahitaji yao, kisha kuwajulisha kwa Yesu, NAD ilipanda zaidi ya makanisa 400 katika mwaka mmoja pekee (2023).
Idadi ya wanachama wa divisheni sasa imekua hadi 1,287,739. Kuanzia 2022 hadi sasa, takribani watu 205,000 wamekubali hadharani kumfuata Kristo kupitia ubatizo, wakiwemo vijana 1,215 katika makambi ya kimataifa ya 2024 Believe the Promise International Pathfinder Camporee huko Gillette, Wyoming.
Mwaka 2024, viongozi wa divisheni walitafakari juu ya ahadi ya Biblia kwamba Roho wa Mungu angeonekana wazi katika siku za mwisho za dunia, kama ilivyokuwa katika siku ya Pentekoste (angalia Matendo 2). Hivyo, wakabuni wazo la Pentekoste 2025 — mwaliko wa NAD kwa viongozi na washiriki wa kanisa kuandaa angalau mipango ya matangazo 3,000 kote katika divisheni.
Kwa neema ya Mungu, makanisa na shule 5,200 yalisajiliwa kushiriki na wanashiriki katika njia za ubunifu za uinjilisti katika maeneo yao.
Pentekoste 2025 ni ukumbusho kwamba kazi ya kuzidisha sio ya viongozi wa kanisa pekee; kila mshiriki ameitwa kutumia vipawa na maeneo yao ya ushawishi kufanya wanafunzi wanaofanya wanafunzi wengine.
Ripoti hiyo iliwatia changamoto watazamaji kutafakari jinsi wanavyoweza kutumia mbinu za ubunifu za kufikia watu, majukwaa ya kidigitali, na mbinu za jadi kusambaza habari njema katika Amerika Kaskazini na zaidi.
Sura ya 2: Nguvu ya Vyombo vya Habari
Ripoti iliwakumbusha watazamaji kwamba kanisa limekuwa mstari wa mbele katika teknolojia tangu maono ya Ellen White ya kuanzisha gazeti dogo ambalo lingesambaa duniani kote. Wakati wa janga la COVID-19, dunia iliingia kwenye kufungwa, lakini makanisa yetu yaliingia mtandaoni, na nafasi ya kidijiti ikawa njia ya uzima. Makanisa kadhaa yaliyo kuwa hayajawahi kurusha ibada mtandaoni hapo awali yalibadilika na kuanza kuwafikia maelfu kupitia mtandao. Leo, makanisa yanaendelea kutoa huduma za ibada ana kwa ana pamoja na huduma za mtandaoni.
Huduma ya vyombo vya habari iliendelea kustawi, huku It is Written, Sauti ya Unabii (Voice of Prophecy), Breath of Life, Faith for Today, Jesus 101, La Voz de la Esperanza, na Life Talk Radio zikiendelea kutoa vipindi vipya na mipango ya uinjilisti inayowaongoza watu wanaotafuta ukweli. Hope Channel Canada pia ilizinduliwa mwaka 2024, na kufikia zaidi ya watazamaji milioni moja.
Tangu mwaka 2022, NAD imeendelea kufikia watu wengi kwa mtandao. Mpango wa Wanafunzi wa Kidijitali 10,0000 ulizinduliwa mwaka 2021, ukiwahimiza washirikali kutumia nguvu ya mitandao ya kijamii na uinjilisti wa kidijitalii kuwafikia watu pale walipo — mtandaoni. Mipango ya maombi mtandaoni pia ilipanua alama ya kidijitali ya kanisa, huku mibofyo ikisababisha kuunganishwa kwa watu na hata kitabu cha rasilimali, [https://www.dmissionary.com/], kilichoandikwa na Justin Kim, mkurugenzi wa uinjilisti wa kidijitali wa Konferensi ya California ya Kati ya Waadventista wa Wasabato.
Ripoti pia iliangazia Tamasha la Filamu la Sonscreen, tamasha la kila mwaka la filamu la divisheni kwa watengeneza filamu vijana. Sonscreen ilianzishwa mwaka 2002, wakati viongozi wa NAD walipotambua nguvu ya simulizi na haja ya nafasi za ubunifu. Kwenye tamasha hili, wanafunzi wa vyuo na vyuo vikuu hushiriki hadithi za maisha yao, changamoto, na imani yao kila mwaka kupitia filamu. Sonscreen Films pia hutengeneza filamu zenye maadili kwa kushirikiana na taasisi za elimu ya juu za Waadventista na mashirika ya kanisa la kimataifa, ikiwa ni pamoja na Hope Media Europe.
“Hadithi hubadilisha mioyo, na tunatumia filamu kusikiliza, kujifunza, na kufundisha masomo kupitia simulizi kama alivyofanya Yesu,” ripoti ya video ilihitimisha.
Sura ya 3: Kulea kwa Ajili ya Baadaye
Sura inayofuata ya ripoti ililenga kwenye uleaji (mentorship), ikieleza kwamba NAD inatambua kuwa mafanikio endelevu ya kanisa letu yako mikononi mwa vijana. Juhudi za kulea vijana zinazojumuisha Pathfinders, mafunzo ya uongozi kwa vijana, huduma katika vyuo vya umma, shule, taasisi za elimu ya awali, vyuo na taasisi za elimu ya juu, mipango ya huduma za NextGen, pamoja na uleaji na mafunzo kutoka kwa viongozi wa divisheni zilionyeshwa kupitia picha na video kutoka maeneo mbalimbali ya NAD.
Moja ya mipango ya sasa ya kulea vijana ya NAD, NextGen, inayolenga kuwatambulisha vijana kwenye nafasi za huduma na kuwawezesha wale wanaohisi wito wa kufanya kazi ya kanisa, iliangaziwa. NextGen inapeleka kipaumbele katika kuwafikia vijana kwenye matukio makuu ya divisheni, ikiwemo Pathfinder Bible Experience na International Pathfinder Camporee.
Eneo lingine muhimu lililotajwa katika uleaji ni vikundi vya mafunzo (training cohorts) ambavyo vinaandaa na kuwawezesha viongozi wengi wa konferensi, yunioni, na divisheni ambao ni wapya katika nafasi zao katikati ya mabadiliko makubwa ya uongozi tangu 2021. Lengo ni kuwaandaa vijana na viongozi wa sasa kusimama imara katika imani yao wanapomtumikia Mungu. Kama ilivyoshirikishwa kwenye ripoti ya video, juhudi hizi zinazaa matunda kwenye vyuo, makanisa na sehemu za kazi kote divisheni.
Sura ya 4: Imani Katika Vitendo
NAD inajitahidi kuonyesha imani katika vitendo kupitia miradi yake ya huduma za jamii, mifumo yake ya afya, na huduma za umishonari za ndani na nje ya nchi, na ilitoa mifano kadhaa ya hili katika ripoti. Kwa mfano, wakati wa janga la COVID-19, juhudi za kufikia jamii ziliongezeka, na zaidi ya mikutano 1,500 kufungua vituo vya kugawa chakula. Vilevile, viongozi wa Huduma za Jamii za Waadventista (Adventist Community Services) walitoa msaada muhimu wa dharura, ikiwemo huduma za kiroho, baada ya vimbunga, mauaji ya risasi, moto wa nyika, na matukio mengine katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Mifumo mitano ya huduma za afya ya divisheni iliendelea kutoa uponyaji wa jumla katika kipindi hiki. Kufikia mwaka 2025, mifumo hii inajumuisha zaidi ya hospitali 100, ofisi za matibabu 2,700, vituo vya huduma za dharura, kliniki za wagonjwa wa nje, na vituo vya upasuaji. Kupitia utafiti wao, uchunguzi wa afya, na upasuaji, wanaonyesha imani katika vitendo, wakitoa huduma bora na huduma yenye huruma katika mwanga wa huduma ya uponyaji ya Kristo.
Ripoti ilizingatia kwa undani msisitizo mkubwa wa NAD kwenye kazi ya umishonari, ikiwemo kutaja maelfu ya wamishonari wanaotumwa kila mwaka ulimwenguni na ndani ya divisheni yenyewe. Na kote Amerika Kaskazini, divisheni inafanya jitihada kufikia zaidi ya makabila na mataifa ya asili 1,200. Kwa mfano, mwezi Machi 2025 uliashiria uzinduzi wa kituo cha kwanza cha redio cha FM chenye nguvu kamili cha Diné Adventist Radio — KDHH 89.5 FM, kilichoanza kurusha matangazo moja kwa moja kuwafikia wasikilizaji katika Jiji la Tuba, Kaibeto, na Western Agency ya Taifa la Navajo. Mradi huu wa kipekee unaolenga kuwafikia watu wa Navajo na ujumbe wa Waadventista wa Sabato kuhusu tumaini, afya, na uponyaji ulitimia baada ya miaka ya maandalizi.
Huduma nyingine muhimu kwa jamii za Wenyeji, Shule ya Asili ya Mamawi Atosketan, ilizindua rasmi ujenzi katika kipande cha ardhi kwenye eneo la hifadhi ya Wenyeji linalojulikana kwa ujasiri na ubunifu. Kituo kipya cha ushawishi, Kituo cha Mamawi Atosketan, kinaangaliwa kama mwendelezo wa kazi ya upainia ya shule hiyo tangu mwaka 2003 katika kuungana na kufanya kazi na watu wa asili.
Imani katika vitendo iliyoonyeshwa kwenye ripoti ilijumuisha takwimu za zaka. Kote katika divisheni, zaka kuanzia 2022 hadi 2024 ilifikia dola bilioni 3.85. Wanachama walitoa zaidi ya matarajio, na ukarimu wao uliendelea hadi kwenye sadaka maalumu kwa ajili ya Pentekoste 2025. Baada ya mpango huu wa uinjilisti kutangazwa mwaka 2024, michango ya wanachama ilifikia dola 543,667 — ushuhuda halisi wa ukarimu na dhamira ya wanachama katika kuwekeza katika kusambaza ujumbe wa malaika watatu katika divisheni yao.
Sura ya 5: Hatima ya Pamoja Katika Utume
Mwaka 2025, Kanisa la Waadventista Wasabato Amerika Kaskazini linaadhimisha miaka 40 ya huduma na utume. Kama ilivyoonyeshwa kwenye ripoti, divisheni iko pamoja katika utume — kwa umakini wa hali ya juu na kupitia nguvu za Mungu na Roho Mtakatifu, divisheni inashiriki habari njema kwa kizazi hiki.
Mungu amekuwa akifanya kazi kwa njia kuu kupitia viongozi na washiriki wa NAD. Kuanzia kupanda makanisa madogo hadi makambi makubwa, kutoka uinjilisti wa kidigitali hadi huduma za jamii, mikutano ya maombi ya kila wiki hadi jikoni za supu, kila mshiriki anashiriki nafasi muhimu katika kutimiza agizo la Injili.
Video ilihitimisha kwa uthibitisho huu: “Utume haupungui kasi. Unakua. Tuko pamoja katika utume. Mwito ni wetu. Tutakwenda.”
Makala ya asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Divisheni ya Amerika Kaskazini. Kwa taarifa zaidi kuhusu Kikao cha Konferensi Kuu cha 2025, ikiwa ni pamoja na masasisho ya moja kwa moja, mahojiano, na simulizi za wajumbe, tembelea adventist.news na ufuate ANN kwenye mitandao ya kijamii.






