Kwa mara ya kwanza, Kanisa la Waadventista wa Sabato nchini Laosi limeandaa semina ya uboreshaji wa ndoa kwa wachungaji na wake zao, hatua muhimu katika kuimarisha maisha ya kifamilia na uongozi wa kanisa katika eneo ambako Ukristo bado ni imani ya wachache.
Tukio hilo la siku moja, lenye mada “Upendo Unachukua Muda,” lilifanyika Vang Vieng, mji unaojulikana kwa uzuri wake wa mandhari na mazingira yake tulivu. Wanandoa kumi na sita wa kichungaji walikusanyika baada ya mafunzo yao ya kila mwaka ya huduma ili kuwekeza katika ndoa zao na ukuaji wao wa kiroho. Semina hiyo iliongozwa na Phouangmala Kongsengphengphet, mkurugenzi wa Huduma za Familia kwa anisa la Waadventista Kusini Mashariki mwa Asia.
Kupitia vipindi vya maingiliano, washiriki walichunguza kanuni tatu muhimu za ndoa yenye afya na inayomlenga Kristo: mpende Mungu, mpende mwenzi wako na watoto, na jipende wewe mwenyewe. Vipindi hivyo vilisisitiza uhusiano wa kihisia, ukaribu wa kiroho, na zana za vitendo za kudumisha mahusiano imara katikati ya mahitaji ya huduma.
“Mpango huu hauwaungi mkono tu viongozi wetu bali pia unawawezesha kuwahudumia vyema mahitaji yanayokua ya familia katika makanisa na jamii zetu,” alisema Keophetsamone Somphou, rais wa Kanisa la Waadventista nchini Laos. Somphou pia aliongoza sherehe ya upya wa viapo wakati wa tukio hilo, ikiruhusu wanandoa kujitolea tena kwa safari yao ya ndoa na huduma.
Siku ilihitimishwa kwa matembezi ya pamoja, ambayo yaliwapa wanandoa fursa ya kutafakari, kuungana, na kufurahia uzuri wa asili wa mazingira yanayowazunguka. Viongozi walisema kuwa hii ilikuwa kumbusho mahsusi la umuhimu wa mapumziko na kuwa pamoja katika maisha yenye shughuli nyingi za huduma.
Kwa idadi ya ushirika wa takribani 3,400 katika taifa lenye zaidi ya watu milioni 7, Kanisa la Waadventista nchini Laosi linaendelea kukua kwa njia ya misheni ya kina. Likiwa ndani ya Dirisha la 10/40, eneo linalojumuisha Asia na sehemu za Afrika ambako idadi kubwa ya watu hawajafikiwa na injili, kanisa linaweka mkazo katika maendeleo ya uongozi, msaada wa kifamilia, na ufuasi wa kiroho kama misingi ya athari za muda mrefu.
Semina hii ya kuboresha ndoa, inayoungwa mkono na Misheni ya Yunioni ya Kusini Mashariki mwa Asia, ni sehemu ya harakati pana katika Kanisa la Waadventista duniani kote ya kukuza familia zenye afya na kuwawezesha viongozi wanaoongozwa na utume. Kwa kuwajali wale wanaowajali wengine, Kanisa linaweka msingi imara zaidi kwa ukuaji wa kiroho na mabadiliko ya jamii.
Makala asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Divisheni ya Kusini mwa Asia-Pasifiki.