Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Avondale anajiandaa kukimbia takriban maili 155 (kilomita 250) kwa siku tano ili kuchangisha zaidi ya USD $16,000 ($A25,000) kwa ajili ya Baraza la Saratani, kuanzia Julai 31, 2025.
Caleb Morton mwenye umri wa miaka kumi na tisa atakabiliana na Njia Nzima ya Great North kutoka Sydney hadi Newcastle, akiita hili “changamoto yake kubwa zaidi ya kimwili hadi sasa.”
Changamoto hii ilichochewa na kifo cha hivi karibuni cha babu yake.
Takriban miezi miwili iliyopita, nilimpoteza babu yangu kutokana na saratani,” alieleza. “Nilitamani sana kufanya jambo la kunitoa katika hali ya huzuni—na pia kujiunga katika mapambano dhidi ya saratani kwa kutumia kipaji ambacho Mungu amenipa.”
Morton anamuelezea babu yake kama kielelezo cha kujitolea na imani.
“Huenda alikuwa mmoja wa watu waliokuwa wakinipa moyo sana maishani. Nilimwona kama mfano wa Yesu kupitia maisha yake—alikuwa kiongozi mtumishi wa familia yetu na mtu wa kutoa kwa moyo wote. Bado sijafikia hata nusu ya utu aliokuwa nao.”
Ili kujiandaa, Morton ameongeza sana mazoezi yake.
“Nimezoea kukimbia mbio fupi—3km hadi nusu-marathon—lakini nimekuwa nikijisukuma kukimbia hadi 90km kwa wiki, ikiwa ni pamoja na marathon za njia na 50km. Pia nimekuwa nikijifunza kuhusu lishe na ni mafuta gani yanayofaa mwili wangu.”
Njia ya Great North ni njia ya vichakani yenye milima na mabonde, ikiwa na zaidi ya futi 26,000 (metri 8000) za kupanda na kushuka—karibu sawa na urefu wa Mlima Everest. Morton atakimbia takriban maili 31 (kilomita 50) kila siku, akirudi nyumbani kila usiku kupumzika kabla ya kuendelea asubuhi inayofuata.
“Ni ultramarathon tano kwa siku tano,” aliongeza.
Atasaidiwa na baba yake na kundi la marafiki wa chuo kikuu ambao watapika, kuweka vifaa na kumfuata kwa gari na baiskeli.
Lengo la Morton ni kuchangisha fedha kupitia ukurasa wake wa GoFundMe kusaidia utafiti wa saratani na kuwahamasisha wengine njiani.
“Siku zote nimejihisi wa kawaida tu. Lakini nataka watu wajue kuwa hauhitaji kuwa kama shujaa wa ajabu ili kufanya jambo lenye maana. Ukipata ule uwiano mzuri—kile unachopenda, kile unachoweza, na kile kinachowasaidia wengine—unaweza kuleta mabadiliko.”
Imani yake pia ina nafasi kubwa katika safari hii.
“Wakati mwili wako unapoishiwa nguvu, unachobaki nacho ni Mungu. Kukimbia kunanipeleka kwenye nafasi hiyo ambapo lazima nitegemee Yeye kikamilifu.”
Changamoto hii inadhaminiwa na Chuo Kikuu cha Avondale na Mradi wa Lift, ambao wamechangia kugharamia vifaa na gharama za lishe. Taarifa za maendeleo zitashirikiwa kupitia kwenye akaunti yake ya Instagram.
“Ninamwamini Mungu kwa matokeo,” alisema Morton. “Tukifikisha dola 25,000, hilo litakuwa jambo kubwa sana—lakini chochote kitakachopatikana, najua kinatenda mema na kinamheshimu babu yangu.”
Makala asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Divisheni ya Pasifiki Kusini, Adventist Record. Jiunge na Chaneli ya WhatsApp ya ANN kwa habari za hivi punde za Waadventista.
