Kanisa la Waadventista Wasabato nchini Mexico hivi karibuni limehitimisha kampeni yake ya kitaifa ya uinjilisti wa mtandaoni ya kila mwaka, ikiwa ni kilele cha miezi kadhaa ya juhudi zilizoratibiwa na viongozi na washiriki wa kanisa katika kueneza injili mitaani, mijini, na kwa jamii za kidijitali kote nchini.
Ikitiririshwa moja kwa moja kuanzia Septemba 6–13, 2025, kutoka Kanisa la Waadventista la Las Lomas mjini Monterrey, mfululizo huu ulikuwa kampeni ya tano mfululizo ya mtandaoni ya kanisa hilo, iliyopangwa kwa kushirikiana na yunioni tano, au maeneo makuu ya kanisa nchini Meksiko.
Kampeni hiyo, iliyopewa kaulimbiu “Decide Vivir Feliz” (“Amua Kuishi kwa Furaha”), iliendeshwa na Luis Orozco, mkurugenzi wa huduma za vijana wa Yunioni ya Kaskazini mwa Mexico. Kila jioni, Orozco aliwahimiza watazamaji kugundua furaha halisi katika Yesu na Maandiko.
“Furaha hupatikana pale tabia yetu inapoakisi tabia ya Kristo,” Orozco alisema, akiwalenga watazamaji kuelekea furaha inayozidi hisia au hali za maisha. “Yesu aliweza kupata furaha hata pale alipokabiliana na kushindwa. Katika Mungu kuna ushirikiano, nguvu, na utambulisho wa kweli.”
Akitaja uzoefu wake binafsi wa msiba, kupoteza, na changamoto za kimwili, Orozco aliwakumbusha watazamaji kwamba imani kwa Kristo inafanya iwezekane kushinda maumivu.
“Kila tabia yako inapokuwa kama ile ya Yesu, ndivyo utakavyokuwa na furaha zaidi,” alisisitiza, huku mashuhuda ya waumini walioshinda majonzi na magumu yakishirikishwa katika kipindi chote cha juma hilo.
Hadithi za Mabadiliko
Mwisho wa mfululizo huo, zaidi ya waumini wapya 3,500 waliamua kuonyesha hadharani uamuzi wao wa kumfuata Kristo kupitia ubatizo, huku maelfu zaidi wakiendelea kushiriki katika masomo ya Biblia ambayo yatazalisha ubatizo zaidi katika wiki zijazo.
Miongoni mwao alikuwa Alan Cedillo, mwanafunzi wa mawasiliano wa umri wa miaka 19 katika chuo kikuu cha umma cha Monterrey. Baada ya kupambana na msongo wa mawazo na hofu ya kijamii, Alan alihisi wito wa Mungu katika usiku wa saba wa mfululizo huo na kuamua kubatizwa.
“Kati ya changamoto za kibinafsi, nilipata amani na kuhisi Yesu akinibadilisha,” alisema. “Nilihisi utulivu, kuelewa sehemu kubwa ya hofu yangu ya kijamii, na hatua kwa hatua nilianza Kumhisi (Kristo) kama rafiki yangu, mlezi wangu, na mwongozi wangu.”
Mabadiliko hayo yalimchochea kushuhudia katika chuo kikuu chake. Akiwa pamoja na marafiki wa kanisa, alianza kutayarisha mahojiano ya ubunifu kwa njia ya video yaliyowaalika wanafunzi wenzake kutafakari kuhusu maisha baada ya kifo, hukumu, na tumaini linalopatikana katika Kristo. Wakati wa kampeni hiyo, alitia muhuri wa uamuzi wake kupitia ubatizo.
Elsi De Jesús Hernández, mwanafunzi wa shule ya sekondari mwenye umri wa miaka 15, pia alibatizwa pamoja na mama yake. Mara ya kwanza alihudhuria kampeni ya uinjilisti ya mitaani karibu na nyumba ya bibi yake, na kufikia mwezi Mei walikuwa wote wawili wakisoma Biblia pamoja.
"Ilipofika wiki hii ya Decide Vivir Feliz (Amua Kuishi kwa Furaha), nilijua ninataka Yesu awe katika maisha yangu—Yeye amekuwa mwongozi wangu,” alisema Hernández.
Hadithi kama za Elsi na Alan zinaonyesha athari pana ya kampeni hiyo. Maelfu ya watu waliunganishwa kupitia miradi ya uinjilisti ya kijamii, juhudi za uinjilisti za mitaani, na ushiriki wa kidijitali pamoja na makumi ya washawishi Waadventista na wanafunzi wabunifu katika miji mikuu na majimbo mbalimbali nchini Mexico, viongozi wa kanisa waliripoti.
Nyumba za Tumaini Zinaongezeka Kote Nchini
Mfululizo huo wa moja kwa moja uliwafikia karibu watu milioni mbili—hatua ya kihistoria—kupitia YouTube, Facebook, Hope Channel Inter-Amerika, 3ABN Latino, vituo 33 vya redio (ikiwemo mitandao ya kiislamu), na maelfu ya mikutano ya ana kwa ana. Zaidi ya makundi madogo 25,000 na “Nyumba za Tumaini” ziliwalika marafiki na majirani kuangalia pamoja.
Katika Iglesia Adventista Alfa y Omega mjini Monterrey, washiriki 25 kati ya 150 walifungua nyumba zao, huku makundi madogo manne yakitiririsha mfululizo huo kwa pamoja. Kote katika makanisa sita ya wilaya hiyo, mpango huo ulijumuisha Jumla ya Nyumba 80 za Tumaini na vikundi vidogo 20, ambapo wageni 54 walishiriki katika tukio la wiki moja.
“Kinachonijaza furaha zaidi ni kuona jinsi washiriki wanavyokumbatia mtindo huu mpya wa uinjilisti, wakichanganya mbinu za kitamaduni na zisizo za kitamaduni na kutumia kila njia ya mawasiliano iliyo wazi kwa njia bora zaidi,’ alisema Arturo King, rais wa Yunioni ya Kaskazini mwa Mexico.
Yunioni hiyo, ambayo inasimamia zaidi ya washiriki 138,000 katika mikuto 1,193, iliona ongezeko kubwa la uongozi na uhusika wa washiriki katika konferensi zake tisa na viwanja viwili za misheni.
“Kwetu sisi, kampeni hii siyo tu kuhusu kile tunachopitia sasa, bali kuhusu kujenga msukumo mkubwa kwa siku zijazo,” King alisema. “Athari kubwa zaidi ni kwamba washiriki wanawafikia watu wengi kuliko wakati mwingine wowote.”
Kutoka Sebuleni Hadi Maeneo ya Umma
Msukumo huo uliwezeshwa na miezi ya maandalizi kaskazini mwa Meico, ikiwemo msafara wa kinabii uliodhihirisha Danieli 2, Shule za Biblia za Likizo katika bustani na viwanja, na shughuli zilizoongozwa na Pathfinders kwenye vitongoji.
“Tumekuwa tukilipeleka kanisa mitaani, tukitekeleza programu mbalimbali huku pia tukihamasisha mpango wetu wa Nataka Kuishi kwa Afya pamoja na miradi mingine ya kijamii,” alisema King.
Zaidi ya kampeni 70 za ubatizo pia zilifanyika Monterrey mwezi Mei kwa msaada wa Redio ya Waadventista Ulimwenguni (AWR).
Kigezo cha msingi cha mafanikio ya kampeni hiyo, King alieleza, kimekuwa maelfu ya Nyumba za Tumaini kote nchini.
“Ni dhana rahisi: nyumba inayofunguliwa ili kuonyesha mfululizo wa uinjilisti, ambapo watu wanaweza kuunganishwa, kushirikiana na kupata uzoefu wa jumuiya,” alisema. “Watu wengi ambao wasingeenda kanisani walifurahia kukusanyika nyumbani. Katika baadhi ya wilaya, kulikuwa na Nyumba za Tumaini mara nne au tano zaidi kuliko vikundi vidogo.”
Kwa King, Nyumba za Tumaini zinawakilisha fursa na pia wajibu.
“Hii ni dirisha la fursa tulilonalo sasa hivi,” alisema. “Mambo yanaweza kubadilika haraka, lakini lazima tutumie kila njia ya mawasiliano na kila mazingira yaliyopo kuwafikia wale ambao bado wanahitaji kusikia ujumbe wa wokovu.”
Maisha Yaliyobadilishwa Kote Meksiko
Katika viunga vya Monterrey, María del Carmen Cortez na mumewe, Rafael González, walifungua nyumba yao kwa ajili ya mfululizo huo baada ya kualikwa na kiongozi wa kikundi kidogo. Kufikia usiku wa nne, majirani walijaa mitaani, wakiimba, wakiangalia kipindi, na kushiriki chakula cha jioni cha tamales na tortillas.
“Shuhuda ziligusia changamoto halisi zinazowakabili watu kila siku na zikachochea mazungumzo yaliyofungua mlango wa ufuasi,” Cortez alisema.
Kulingana na Sergio Arévalo Delgado, mchungaji anayeongoza wilaya ya Juárez Norte ambako Cortez anaishi, kikundi hicho sasa kitaandaliwa kama kikundi kidogo, huku kadhaa wakiwa tayari wanashiriki katika masomo ya Biblia na mipango ikiendelea ya kuwaunganisha watoto na vilabu vya Adventurer na Pathfinder katika kanisa la karibu.
Huko Catemaco, Veracruz, Carmen Prados—aliyewahi kuwa muchawi maisha yake yote—aliandaa Nyumba ya Tumaini pamoja na mumewe, Salomón. Tangu alipobatizwa miaka mitatu iliyopita amekuwa mshiriki hai katika kanisa lake la mahali, akifundisha masomo ya Biblia na kuongoza masomo ya Biblia katika vikundi vidogo kadhaa. Yeye ni mmoja wa viongozi wa vikundi vidogo zaidi ya 9,200 na wenyeji wa Nyumba za Tumaini 4,700 katika eneo la Yunioni ya Inter-Oceanic Mexico, waliojitolea kwa ufuasi unaoendelea mwaka mzima.
“Kampeni hii imetukumbusha tusipoteze muda,” alisema. “Lazima tusambaze habari njema kwamba unaweza kuishi kwa furaha katika Yesu, bila kujali mapambano au changamoto ambazo adui analeta.
Kwa Darnelly Chablé jijini Mexico City, kampeni hiyo ilizidisha kujitolea kwake kwa huduma baada ya yeye, mumewe, na mwana wao mwenye uhitaji maalum kubatizwa mapema mwaka huu. Alipojifunza zaidi kuhusu kampeni ya kitaifa ya mtandaoni, alianza kuipigia debe kupitia akaunti zake za mitandao ya kijamii pamoja na za mwanawe, na hatimaye akaamua kuandaa Nyumba ya Tumaini katika chumba kikubwa ambako takribani familia kumi zenye watoto wenye uhitaji maalum walijumuika kila jioni kutazama mfululizo huo.
“Watu wanaonifuata wamekuja kila usiku, wengi wakiwa na mahitaji makubwa ya kihisia,” alisema. “Ushuhuda wangu wa jinsi Mungu alivyorudisha ndoa yangu umeimarisha azma yangu ya kuendelea kuwafikia wengine.”
Akiwa na msaada wa kanisa lake la mahali, ameahidi kuendelea kuwafikia watu wapya kupitia Nyumba ya Tumaini aliyoiandaa.
Huko Tuxtla Gutiérrez, Chiapas, Delfino Grajales na familia yake waliandaa watu 30, zaidi ya nusu wakiwa wageni, katika ua wao kila usiku. Baada ya kila mkutano, kikundi kilishiriki chakula na ushirika, kikiimarisha urafiki na imani. Hata meya wa mji huo, Enrique Nájera Reyes, alihudhuria pamoja na mkewe.
“Ninajisikia furaha sana kurejea katika njia za Bwana pamoja na familia yangu,” alisema Nájera. “Ni heshima kushiriki katika mikutano hii, ambapo mtu anahisi kama sehemu ya familia na anaweza kushirikiana na ndugu na marafiki, huku pia akitimiza misheni ya Yesu.”
Nyuma ya Pazia na Zaidi
Kila jioni, kipindi cha saa moja kilijumuisha muziki wa asili, maombi, shughuli za watoto, na vipengele vifupi vilivyoangazia afya, fursa, vijana, uchapishaji, na huduma za akina mama. Zaidi ya watu 60 walishirikiana katika uzalishaji pamoja na mamia ya wajitoleaji waliokuwa wakiendesha vituo vya kupiga simu, kusimamia kampeni za masoko, na kuratibu juhudi za kufikia watu mtandaoni.
Matokeo yalikuwa ya kushangaza, viongozi walisema: jumbe 900 kupokelewa, usajili 145 wa masomo ya Biblia, karibu maombi ya sala 500, na makumi ya simu za ufuatiliaji. Vipindi 33 vya redio—vikiwemo vituo sita vya kibiashara—vilitangaza mfululizo huo bila gharama, huku akaunti 12 za mitandao ya kijamii zikiongeza ufikikaji wake kote nchini. Programu ya Esperanza México Radio ilipata wastani wa miunganisho 150 mubashara kila usiku na tayari imepita upakuaji 17,000.
Sasa ikiwa katika mwaka wake wa tano, kampeni hiyo ya mtandaoni imezidisha mara mbili matokeo ya ubatizo tangu 2021, ikipita ubatizo 55,400 kufikia Septemba 13, huku zaidi yakitarajiwa.
Viongozi wa kanisa walipongeza matokeo na maono mapya ya uinjilisti.
“Tunataka kutoa msukumo mkubwa kwa uinjilisti wa kidijitali, hasa redio ya mtandaoni,” alisema King. “Uongozi huko Mexico umeungana, na tunaamini ni kazi ya Roho Mtakatifu. Hatupo hapa kushindana bali kuongezea.”
Abraham Sandoval, rais wa Yunioni ya Inter-Oceanic, alikubaliana.
“Wakati mwingine katika makanisa yetu tunatia shaka kuhusu athari za mitandao ya kijamii, lakini ripoti hii inaonyesha upeo mkubwa na matokeo. Tunashukuru kwa yale yaliyofanywa,” alisema.
Mchungaji Ignacio Navarro, rais wa Yunioni ya Chiapas, alisema uwezo ni mkubwa sana: “Mexico ina washiriki 850,000, ikiwakilisha familia 200,000. Ikiwa kila familia itakuwa Nyumba ya Tumaini, tunaweza kufikia lengo hilo hivi karibuni. Namrudishia Mungu utukufu kwa kazi hii kubwa mno, na naamini tutakuwa hata wenye nguvu zaidi tunapoendelea mbele.”
Kuanzia mawimbi ya redio hadi sebule za nyumbani, kutoka mabango ya barabarani huko Monterrey hadi mwaliko kupitia WhatsApp katika miji midogo, viongozi walisema kampeni hiyo inaakisi enzi mpya ya misheni.
“Tunaamini Mungu analisogeza kanisa Lake nchini Mexico kuelekea jambo kubwa sana,” alisema King.
Mipango tayari imeanza kwa ajili ya kampeni ya kitaifa ya uinjilisti wa mtandaoni ya mwakani, iliyopangwa kuandaliwa kutoka Yunioni ya Kusini Mashariki mwa Mexico mnamo Agosti 2026.
Helena Corona, Gaby Chagolla, Martín Olvera, César Martínez, na Yosainy Colina walichangia taarifa hii. Makala asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Divisheni ya Inter-Amerika. Jiunge na Chaneli ya WhatsApp ya ANN kwa habari za hivi punde za Waadventista.















