Angela Brown hakuweza kuacha tabasamu alipovikwa medali, akiheshimiwa kwa miaka yake 28 ya uaminifu katika kueneza injili kupitia huduma ya uinjilisti wa vitabu.
Alikuwa miongoni mwa wahudumu zaidi ya 350 wa uinjilisti wa vitabu (LEs), au makolportea, waliotambuliwa wakati wa Kongamano la Huduma za Uchapishaji la Divisheni ya Inter-Amerika (IAD) lililofanyika Mjini Panama, Panama, Machi 23-25.
“Mungu amenibariki sana katika huduma hii,” alisema Brown, akitafakari safari yake. Kutoka kufanya kazi kiwandani nchini Jamaika alikozaliwa, kumtunza mumewe mgonjwa, na kulea watoto watatu, hadi siku moja kujifunza kuhusu fursa za kolportea kanisani kwake—alimtumainia Mungu kwa yote yaliyofuata.
“Mimi na Mungu tumekuwa katika huduma hii kwa muda mrefu,” alisema Brown. “Kazi hii ni shauku yangu.”

Akiwa mhudumu hai wa uenezaji wa vitabu, ameweza kuwapeleka watoto wake watatu katika shule za Waadventista na kupata fursa ya kusafiri katika nchi nyingi.
“Sio kuhusu pesa,” alisema. “Ni zaidi ya hilo. Ni kuhusu kumtumainia Mungu maishani mwako. Ni kuhusu kuungana na watu na kushiriki vitabu vinavyoweza kufungua mlango wa injili kubadilisha maisha yao,” alieleza Brown.
Brown ndiye aliyefanya mauzo mengi zaidi katika IAD mwaka 2024, akiuza zaidi ya dola za Marekani 13,500 kupitia vitabu vya Chama cha Uchapishaji cha IAD (IADPA). Pia alitunukiwa nafasi ya tatu wakati wa kongamano hilo kwa kuwaongoza waumini wapya 86 kubatizwa mwaka 2024.

Harakati Inayokua
Kwa mujibu wa waandaaji, Brown alikuwa miongoni mwa wainjilisti wa vitabu 2,615 wa kawaida, wa muda na wanafunzi walioko katika yunioni 20 za IAD ambazo zimewekwa chini ya Huduma za Uchapishaji na IADPA—nyumba kubwa zaidi ya uchapishaji katika divisheni hiyo. Yunioni tano za Mexico ziko chini ya nyumba ya uchapishaji ya GEMA, ambayo inasimamia wahudumu 2,377.
Kongamano la hivi majuzi lilithibitisha tena ahadi ya Huduma za Uchapishaji za IAD na IADPA ya kuwawezesha, kuwahamasisha na kuwapatia rasilimali—za kuchapishwa na za kidijitali—ili kutangaza ujumbe na kutoa tumaini kwa wahudumu wa uinjilisti wa vitabu na wale wanaoshiriki injili kupitia vitabu vya Waadventista.

“Tunataka kuendelea kuwahamasisha kutimiza utume, kutambua wahudumu bora miongoni mwenu, kushiriki muda na wengine kama ninyi, kutoa taarifa za malengo yaliyoafikiwa, na kufufua tena ahadi yetu kwa Mungu na huduma hii pamoja,” alisema Isaías Espinoza, mkurugenzi wa Huduma za Uchapishaji wa IAD.
Kongamano hilo, lenye kauli mbiu "Wateuliwa Kutangaza Kurudi Kwake Duniani," lilikuwa la kwanza katika eneo la IADPA. Ni sehemu ya mpango unaoendelea tangu 2021 wa kupanua Huduma za Uchapishaji, ikijumuisha wahudumu wa kudumu, wa muda (saa 5 hadi 20 kwa wiki), na wanafunzi wanaosaidia masomo yao. Aidha, Huduma za Uchapishaji zinasimamia wakurugenzi wa uchapishaji wa makanisa ya ndani ambao huwapatia wanachama na LEs watarajiwa rasilimali.

Kwa miaka mingi, wainjilisti wa vitabu walifanya kazi kwa kujitegemea, lakini tangu mwaka wa 2021 idadi yao imeongezeka mara mbili kutokana na msaada wa yunioni na IADPA, alieleza Espinoza.
“Wainjilisti wa vitabu ni wajumbe wa tumaini,” alisema. “Wameitwa kupeleka injili mahali ambapo wahubiri hawawezi kufika, wakipanda mbegu zitakazogusa mioyo ya wasomaji. Ili kutimiza utume wa Mungu, lazima tuendelee kuandikisha zaidi kwa huduma hii adhimu.”
Mfano wa Ukuaji
Tangu 2019, Huduma za Uchapishaji katika Konferensi ya Yunioni ya Dominika (DUC) zimeongeza juhudi zao maradufu. Yunioni hiyo sasa iko miongoni mwa tatu bora katika IAD, ikiwa na wainjilisti wa vitabu (LEs) 248, wakiwemo 106 wa kudumu—ongezeko kubwa kutoka wainjilisti 15 tu waliokuwa hai miaka sita iliyopita, alisema Roberto Matos, mkurugenzi wa Huduma za Uchapishaji wa DUC.
“Uinjilisti wa vitabu ulikuwa hai sana miaka ya 1990, ikiwa na wainjilisti zaidi ya 300, lakini mpango ulipobadilika na faida kupungua, idadi ilishuka haraka sana,” alisema Matos.
Leo hii, motisha mbalimbali, zikiwemo mikopo ya awali, zinazoendelea kuwasaidia wainjilisti wa vitabu.
“Tumekuwa tukiendesha mafunzo endelevu katika viwanja (fields) vyetu vyote na kuandikisha washirika kila robo mwaka katika makanisa na wilaya, jambo ambalo limeimarisha huduma hii,” aliongeza.
Matos pia alieleza kuwa mara moja kwa mwaka, kundi la wahubiri wa vitabu wenye vipawa vya uinjilisti husafiri kwenda eneo maalum kwa wiki kadhaa ili kuandikisha, kutoa mafunzo, kuuza vitabu, na kufanya kampeni za uinjilisti.
“Uzoefu wa moja kwa moja hujenga umoja, lengo la pamoja, na kujitolea zaidi kwa utume wa huduma ya uchapishaji,” alifafanua.
Athari kwa Kanisa la Ndani
DUC ina wakurugenzi 976 wa uchapishaji katika makanisa ya ndani, moja ya idadi kubwa zaidi katika IAD. Viongozi wanalenga kufikisha wainjilisti 200 wa kawaida ifikapo 2028, alisema Matos.
“Kufikisha wainjilisti 200 inaonekana ni lengo la wastani, lakini lazima tuendelee kuboresha mbinu zetu ili kuifanya huduma hii kuwa ya kitaaluma na kuhakikisha kila mmoja anajitolea kusalia katika uinjilisti wa vitabu,” alieleza.
Katika Misheni ya Yunioni ya El Salvador, ikiwa na jumla ya wahudumu 64, huduma ya uchapishaji imepanuka hadi kufikia wakurugenzi 878 wa uchapishaji wa makanisa ya ndani.
“Wale wakurugenzi 878 wa uchapishaji wa makanisa ya ndani ni wa muhimu kwa sababu ni ndugu na dada wanaohamasisha washiriki wa kanisa kununua vitabu,” alisema Evila Lazo, mkurugenzi wa Huduma za Uchapishaji wa Misheni ya El Salvador.
Mauzo mengi hufanyika katika ngazi ya ndani, alisema. Mikutano ya robo mwaka, mafunzo, na mikusanyiko ya kitaifa imekuwa muhimu katika kupanua Huduma za Uchapishaji nchini.

Huduma Inayobadilisha Maisha
Kwa Rosa Elena López, mwenye umri wa miaka 38 kutoka El Salvador, ambaye alishika nafasi ya pili kati ya wainjilisti wa vitabu watatu bora waliotumia kiasi kikubwa zaidi kununua kutoka IADPA mwaka 2024, kuwa sehemu ya huduma ya uinjilisti wa vitabu kwa miaka 15 iliyopita kumebadilisha maisha yake kabisa.
“Kwa kweli, huduma hii imebadilisha maisha yangu kwa njia ya ajabu,” alisema López.

“Kila mauzo, kila kitabu kinachoingia nyumbani, ni muujiza kutoka kwa mkono na uongozi wa Roho Mtakatifu. Mimi ni chombo tu, natoka kila siku, nikimtegemea Mungu, nikiwa na vitabu vyake.”
Kuuza vitabu kulimhamasisha Rosa Elena López kuboresha ujuzi wake wa kusoma, kwani alikuwa na elimu ya msingi tu.
“Katika huduma hii nina muda wa kuwasikiliza watu, kujua changamoto zao, kujenga mahusiano, na kutoa vitabu vinavyoweza kusaidia,” alisema. Hata watu wasiponunua vitabu vyake, anajenga urafiki na kumwachia Mungu afanye kazi. “Wateja wengi na watu ninaokutana nao huomba sala, hivyo huwaweka kwenye orodha yangu ya maombi kila wiki.”

Anashiriki vitabu kwenye lifti, vituo vya basi, na popote Mungu anapomwongoza.
Byron Pérez hakuwahi kufikiria kuwa Mungu angebadilisha maisha yake kupitia huduma ya uenezaji wa vitabu. Alikulia kijijini kusini mwa Guatemala ambako lugha ya Mam, lahaja ya Kimaaya, ilizungumzwa, na alikuwa akifanya kazi ya ujenzi kwa miaka 12. Kila kitu kilibadilika alipoalikwa na kiongozi wa kanisa kuhudhuria mkutano wa uinjilisti wa vitabu.
“Nilivutiwa na fursa hiyo, nikaacha yote nyuma,” alisema Pérez.
Akiwa na elimu ya darasa la sita tu, Pérez alijua anahitaji kujijengea kujiamini, hivyo alimaliza shule ya sekondari na kupata shahada ya saikolojia ya kliniki.
“Ilinichukua miaka 13 kujiandaa kielimu, na leo nina ujasiri wa kuingia ofisi za biashara, kuendesha semina za afya ya akili, na kushiriki vitabu vinavyoweza kubadilisha maisha,” alisema.

Mwaka jana, aliuza vitabu vyenye thamani ya Dola za Marekani 11,000. Mafanikio haya yalimfanya Pérez kushika nafasi ya nne kati ya wauzaji bora wa vitabu katika divisheni nzima.
Huduma ya uinjilisti wa vitabu imefungua milango kwa Pérez na familia yake, ikamwezesha kuwasomesha watoto wake. Amezungumza na mamia ya walimu na maafisa wa serikali chini ya Wizara ya Elimu, akiwapatia mashauriano ya kiafya bila malipo kwa wale wanaonunua vitabu anavyovipendekeza.

“Huduma ya uinjilisti wa vitabu ilinilipia masomo yangu yote,” alisema Pérez. “Nilikuwa nikitembea mtaa kwa mtaa nikiwa na seti yangu ya vitabu, na siku moja nilianguka mtoni na vitabu vyote vikaharibika. Nikamwambia Mungu, 'Kuanzia sasa, nitajaribu kuuza vitabu zaidi, lakini itakubidi unipe gari, maana siwezi tena kubeba vitabu kwenye mabasi, mitaani, na kuvuka mito.’ Sasa Mungu amenibariki na gari, na ninaweza kuwafikia watu wengi zaidi. Hii ni kila kitu kwangu. Sio kazi tu, bali ni safari ya kuleta tumaini na amani ambayo ni Yesu pekee awezaye kutoa,” alisema Pérez.
Mtazamo Mpana
Brown, López, na Pérez ni miongoni mwa mamia ya wainjilisti wa vitabu waliojitolea katika Divisheni ya Inter-Amerika (IAD), ambao wameahidi kutimiza utume kila siku, alisema Espinoza. Tukio hilo, lililofanyika Machi 23–25, 2025, pia lililenga kuwahamasisha wainjilisti wa vitabu kuongeza juhudi zao ili kuwafikia watu wengi zaidi kwa ajili ya ufalme wa Mungu.
Hadi sasa, muundo wa huduma ya uchapishaji wa IAD umezaa wakurugenzi wa uchapishaji wa makanisa ya ndani takriban 8,000 wanaotoa rasilimali za uinjilisti wa vitabu miongoni mwa waumini.
“Kanisa linawahitaji viongozi hawa wa ngazi ya kanisa la ndani,” aliongeza Espinoza.

Almir Marroni, mkurugenzi wa Huduma za Uchapishaji wa Konferensi Kuu, aliwapongeza viongozi wa kanisa waliorejesha uhai katika huduma zao za uchapishaji na kuhamasisha yunioni zingine kuimarisha msaada wao kwa wainjilisti wa vitabu.
“Lazima muwe na maono, uongozi thabiti, vitabu vya kutosha, wainjilisti wa kujitolea, na sera wazi,” alisema.
Marroni alisisitiza kuwa kuandikisha, kutoa mafunzo, na kuimarisha wainjilisti wa vitabu ni muhimu kwa ukuaji wa kanisa.
“Wainjilisti wa vitabu ni mashujaa wasioonekana waliolinda mpango wa Mungu katika historia yote ya Biblia.” Akihutubia mamia ya waliokusanyika, aliwakumbusha jukumu lao muhimu: “Mmechaguliwa na Mungu kubadilisha maisha na kutimiza ahadi zake katika nyakati hizi za changamoto.”

Alibainisha kuwa kanisa la kimataifa linarejea kwenye misingi ya uinjilisti wa vitabu na alikiri jitihada za Divisheni ya Inter-Amerika kama mfano unaokua kwa wengine duniani kote.
Mwito wa Kuchukua Hatua
Rais wa IAD, Elie Henry, alisifu kujitolea na uaminifu wa wainjilisti wa vitabu katika eneo lote.
“Nawapongeza kwa kuendelea mbele licha ya changamoto—mkiwaletea Kristo watu majumbani, mkiwaombea familia, na kubadilisha maisha,” alisema. “Ninyi ni wamisionari wa kweli. Endeleeni kusonga mbele, nyumba hadi nyumba, mitaani, na katika miji mikubwa.”
Henry aliwahimiza wainjilisti wa vitabu waendelee kuhudumu kwa huruma na shauku ili kusaidia kupunguza mateso ya wanadamu.
Wakati wa kongamano hilo, IADPA ilithibitisha tena kujitolea kwake kuwaunga mkono wainjilisti wa vitabu kwa kutoa mamia ya rasilimali kusaidia utume wao.
“Tumejitoa kutoa lishe ya kiroho kwa nchi 36 zilizo ndani ya divisheni yetu,” alisema Saul Ortíz, rais wa IADPA.

Ortíz alieleza kuhusu upana na miundombinu ya IADPA, ikiwa ni pamoja na makao makuu yake Miami, maduka 91 ya vitabu katika eneo lote, na shughuli katika sarafu 18 tofauti.
“Timu yetu ya watu 205 imejitolea kwa utume huo huo kila siku,” aliongeza.
Mbali na medali zilizotolewa kwa wainjilisti wa vitabu na hafla ya kuwakabidhi beji, wakurugenzi wa uchapishaji wa yunioni walitambuliwa kwa juhudi zao kukuza uinjilisti wa vitabu makanisani na katika maeneo yao.
Kongamano lilipofikia tamati, Marroni aliheshimiwa kwa uongozi wake wenye matokeo na msaada thabiti kwa IAD. Wajumbe walifufua tena ahadi yao ya kuacha nuru ya injili iwaongoze wanapoendelea kutimiza utume wa kanisa kupitia vitabu na machapisho ya Waadventista.
Makala asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Divisheni ya Inter-Amerika. Jiunge na Chaneli ya ANN ya WhatsApp kwa sasisho za hivi punde za habari za Waadventista.