Huduma ya Rekodi za Kikristo inayojulikana kama Christian Record Services, Inc. (CRS) inafuraha kutangaza uteuzi wa Cesar Perozo kama rais wake mpya, kufuatia utafutaji wa kitaifa uliofanywa na FaithSearch Partners.
Akiwa na uzoefu wa zaidi ya miaka 25 katika huduma ya kichungaji na uongozi wa kiutawala, Perozo analeta utaalamu mkubwa katika usimamizi wa kimkakati, rasilimali watu, na ushirikiano wa kimataifa. Nafasi zake za awali ni pamoja na makamu wa rais wa utawala na mkurugenzi wa rasilimali watu wa Konferensi ya New England Kusini, ambapo alisimamia bajeti na kuongoza mipango ya upandaji makanisa, ulinzi wa watoto, na maendeleo ya shirika.
Hivi karibuni, Perozo alihudumu kama mchungaji wa makanisa ya Upward na Fairview huko North Carolina, Marekani, ambapo alianzisha vituo vya usambazaji wa misaada ya maafa, alikusanya fedha kwa miradi ya kanisa na shule, na aliongoza huduma za Shule ya Sabato katika Konferensi ya Carolina.
“Tunafurahi kumkaribisha Mchungaji Cesar Perozo katika urais wa Huduma ya Rekodi za Kikristo (Christian Record Services),” alisema G. Alexander Bryant, mwenyekiti wa bodi ya CRS. “Ana shauku ya kumtumikia Bwana na amejiandaa kwa huduma ya kueneza injili kwa wale ambao ni vipofu na wenye uoni hafifu. Nina hamu ya kuona uongozi ambao Cesar ataleta katika huduma hii na kutazamia kuona ikipiga hatua zaidi.”
“Ni heshima kubwa kwangu kukubali jukumu la kuwa rais wa Huduma za Rekodi za Kikristo,” asema Perozo. “Pamoja na wafanyakazi wetu waliojitolea na jamii thabiti ya wasioona na wenye uoni hafifu tunaowahudumia, natumaini kuendeleza dhamira yetu kwa ari mpya na mshikamano. Nina hamu kubwa hasa ya kuimarisha ushirikiano wetu na Divisheni ya Amerika Kaskazini, tunaposhirikiana kwa dhati ili kuleta athari yenye maana na ya kudumu.”
Kuhusu Huduma ya Rekodi za Kikristo (Christian Record Services)
Huduma ya Rekodi za Kikristo (Christian Record Services, Inc.) ni huduma ya Kanisa la Waadventista wa Sabato yenye makao yake Lincoln, Nebraska, ambayo imekuwa ikihudumia watu wenye ulemavu wa kuona tangu 1899. Kupitia programu kama vile huduma za maktaba ya sauti na maandiko ya braille, makambi ya majira ya joto, vifaa vya masomo ya Biblia, na mipango ya msaada wa jamii, CRS inatoa rasilimali zinazokuza uhuru, elimu, na faraja ya kiroho. Kila mwaka, maelfu kote Amerika Kaskazini hufaidika na huduma zake, ambazo zinawezekana kupitia michango, wajitolea, na ushirikiano na makanisa na mashirika ya ndani.
Makala asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Christian Record Services. Jiunge na Chaneli ya WhatsApp ya ANN kwa habari za hivi punde za Waadventista.
