Mfumo wa nishati wa gridi ndogo unaotumia nishati mbadala sasa unasaidia mahitaji ya umeme ya Kliniki za Kitivo cha Tiba (Faculty Medical Clinics, FMC) cha Chuo Kikuu cha Loma Linda.
Mfumo huo mpya huzalisha megawati mbili za nishati safi na ya kuaminika ya sola moja kwa moja katika eneo la kliniki, na pia unajumuisha mfumo wa kuhifadhi umeme kwenye betri. Tangu ulipoanza kufanya kazi kikamilifu Agosti 22, 2025, mradi huu umeleta akiba kubwa ya gharama za nishati na uimara wa uendeshaji, huku pia ukipunguza athari za kimazingira zinazohusiana na umeme katika FMC.
Mfumo huu mpya umeanza kufanya kazi baada ya miaka mitatu ya upangaji na miezi 18 ya ujenzi. Umeme huzalishwa na paneli 3,622 za sola zilizowekwa katika ghorofa ya juu ya maegesho ya P4 na juu ya eneo la maegesho ya madaktari, na hivyo pia kutoa kivuli kwenye maegesho.
Betri ya Tesla yenye megawati moja, iliyoko upande wa kusini wa jengo, huhifadhi umeme wa ziada na inaweza kutoa umeme wa dharura kwa muda wa saa sita. Mfumo huu pia unaunga mkono vituo 10 vya kuchaji magari ya umeme vilivyoko katika eneo la maegesho upande wa magharibi wa FMC. Kampuni ya Renewable Energy Partners (REP) kutoka Corona, California, ambayo ilijenga mfumo huu, pia itahusika katika matengenezo yake kuendelea mbele.
Shughuli za FMC hutumia wastani wa megawati 1.7 za umeme kwa siku, huku matumizi yakifikia zaidi ya megawati mbili katika miezi ya kiangazi yenye matumizi ya juu. Gridi ndogo ya nishati itatoa asilimia 87 ya umeme unaohitajika wakati wa mahitaji ya juu, na iliyobaki itanunuliwa kutoka kwa Southern California Edison.
Akiba ya gharama kwa kutumia mfumo wa gridi ndogo ya nishati inapatikana kwa kuwa FMC inasimamia kwa ufanisi zaidi chanzo chake cha nishati, jambo linalowezesha upangaji makini zaidi wa bajeti ya gharama za nishati kwa muda mfupi na mrefu.
Gharama ya sasa ya msingi kwa umeme unaonunuliwa kutoka Southern California Edison ni senti 17 kwa kila kilowati saa, na kupanda hadi senti 24 katika nyakati za kilele. FMC imeingia mkataba na kampuni inayoendesha gridi ndogo ya nishati kulipa senti 15 kwa saa kwa miaka 30 ijayo.
Kwa viwango vya sasa, FMC itaokoa dola 500,000 za Kimarekani kwa mwaka. Kwa vile gharama ya umeme inatarajiwa kufikia senti 30 kwa kila kilowati saa wakati wa mkataba, akiba ya kila mwaka inaweza kufikia dola milioni 1.5 za Kimarekani.
“Miundombinu yetu ya paneli za jua inaimarisha uwezo wetu wa kuhudumia jamii, hata wakati wa dharura,” alisema Ricardo Peverini, rais wa Loma Linda University Faculty Medical Group. “Inapunguza athari zetu kwa mazingira, inafanya shughuli zetu kuwa imara zaidi, na inaokoa rasilimali ambazo tunaweza kuziekeza tena katika huduma za wagonjwa. Huu ni mustakabali wenye afya zaidi kwa wagonjwa wetu, wafanyakazi wetu, na eneo letu.”
Makala asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Loma Linda University Health. Jiunge na Chaneli ya WhatsApp ya ANN kwa habari za hivi punde za Waadventista.


