Kanisa la Waadventista wa Sabato huko Chiapas, Mexico, limeanza mafunzo na kuwawezesha wazee wa makanisa ya ndani katika zaidi ya makanisa 3,000, kwa maandalizi ya juhudi kubwa za uinjilisti zenye lengo la kufikia idadi ya kihistoria ya ubatizo ifikapo mwisho wa Aprili.
Takriban wazee 8,000 waliowekwa wakfu walikusanyika katika maeneo mbalimbali katika viwanja (fields) tisa vya kikanda kuanzia Januari 10–18, 2025, ili kutiwa moyo, kufundishwa, na kujitoa zaidi kwa misheni wakati wa athari ya kiinjilisti isiyo na kifani, kwa mujibu wa ripoti ya Ignacio Navarro, rais wa Yunioni ya Chiapas ya Mexico.

"Viongozi wetu, wazee wetu, wako tayari kusonga mbele kwa nguvu chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu ili kupeleka ujumbe wa injili katika kila nyumba, familia, na mtu katika jimbo la Chiapas," alisema Navarro. "Tutaungana kwa siku za athari za uinjilisti katika mwezi wa Februari na Machi, na tutaandaa juhudi kubwa za mavuno ya uinjilisti kuanzia Aprili 19–26 katika makanisa yote ya Chiapas."
Vipindi vya Mafunzo ya Uinjilisti Kote Chiapasi
Msafara wa vipindi vya mafunzo hayo uliwapatia wazee wa kanisa waliowekewa mikono ujumbe wa kiroho, ukiwahimiza kumkaribia Mungu zaidi na kujitoa kwa kina katika utume popote wanapotumikia. Wazee wa kanisa na washiriki hai wa kanisa walikusanyika katika Tapachula, Pueblo Nuevo Solistahuacán, Pichucalco, Palenque, Cintalapa, Tuxtla Gutiérrez, na Comitán.
Kila kipindi kilihudhuriwa na viongozi wa makanisa ya ndani kati ya 700–1,200, wakijifunza kuhusu changamoto za sasa zinazolikumba kanisa, jinsi ya kuwahamasisha na kuwashirikisha washiriki katika uinjilisti kupitia programu na mipango mbalimbali, na mambo mengine.

Vipindi hivi maalum vya mafunzo ya kiinjilisti vilikuwa sehemu ya ajenda ya kimisheni ya eneo lote inayoongozwa na Yunioni ya Ciapas Mexico kwa ushirikiano na Divisheni ya Baina ya Amerika (IAD) ili kuimarisha uenezaji wa injili kwa ajili ya sherehe kubwa ya ubatizo itakayofanyika Tuxtla Gutiérrez, Chiapas, mnamo Aprili 26, 2025.
Viongozi wa kanisa wanakadiria kuwa zaidi ya waumini wapya 38,000 watajiunga na kanisa katika miezi minne ya kwanza ya mwaka huu.
Wakati wa ziara yake huko Chiapas, Balvin Braham, makamu wa rais wa IAD anayesimamia uinjilisti, aliwahimiza wazee wa kanisa kuimarisha ahadi yao pamoja.
"Mungu anawaita muwe sehemu ya kazi hii ya ajabu ya kuwaandaa wengine kwa ajili ya Ufalme wa Mbinguni," alisema Braham. "Tunakuza mpango wa ‘Familia Yote Katika Utume’ na tunaomba kumwagwa kwa Roho Mtakatifu kupitia juhudi hii nzuri. Lengo lilikuwa kuwabatiza watu zaidi ya 20,000 katika miezi minne hii, lakini Yunioni yenu ya Chiapas imeweka lengo la kuwafikia watu 38,612."
Braham alishiriki kwamba mnamo Aprili 26, viongozi wanakadiria kuwa zaidi ya watu 70,000 watabatizwa katika eneo lote la IAD.

Kuwahamasisha Viongozi na Washiriki
Viongozi wa Yunioni walisema hii ni mara ya kwanza kwa kanisa katika Yunioni ya Chiapas Mexco kujaribu kuwahamasisha washiriki wake wengi kwa ajili ya ubatizo mkubwa katika muda mfupi kama huu. Mwaka wa 2024 pekee, takriban watu 23,000 walibatizwa katika makanisa yote ya Chiapas.
“Kila mwaka, yunioni yetu huandaa msafara maalum wa kuwawezesha viongozi wa makanisa ya ndani, lakini mwaka huu, imejikita mahususi katika kuwawezesha wazee wa kanisa na viongozi wa makanisa kupitia mpango wetu wa uinjilisti ‘Tumaini Baina ya Amerika: Mbingu Inakungoja,’" alieleza Navarro.

Vipindi vya mafunzo vya msafara wa uinjilisti vilihusisha ubatizo wa watu 160, matokeo ya juhudi kubwa zilizofanyika mapema Januari. Programu hii ilijumuisha tamasha la muziki na mada kutoka kwa wakurugenzi wa idara za IAD pamoja na viongozi wa utawala na idara wa Yunioni ya Chiapas Mexico.
Washiriki walionyesha furaha yao kwa fursa ya kuwa sehemu ya tukio hili la kihistoria.
Maoni kutoka kwa Wazee wa Makanisa Waliowekewa Mikono
Orbin Gutiérrez, mzee katika Kanisa la Waadventista Wasabato la Copainalá II kwa miaka 30, alishiriki shauku yake.
“Kwangu, hii imekuwa uzoefu mzuri, na namshukuru Mungu kwamba kanisa linatupa fursa ya kushiriki katika tukio maalum kama hili ambapo tunaweza kubatiza katika ngazi ya wilaya. Ni furaha kubwa na heshima.”

Levi Morales wa Kanisa la Waadventista Wasabato la Las Nubes katika Konferensi ya Soconusco, ambaye amewekewa mikono kama mzee kwa mwaka mmoja, alisema hawezi kuelezea hasa furaha anayoihisi kwa kuwa sehemu ya juhudi kubwa ya kiinjilisti.
“Tukio hili la kwanza lilinivutia sana kwa sababu ya uwezeshaji ambao konferensi na yunioni zinatupa kubatiza na kuwakaribisha wale ambao tumekuwa tukishirikiana nao katika masomo ya Biblia kanisani,” alisema Morales.
“Hii ni heshima ambayo kanisa linatupa, na namshukuru Mungu kwa fursa hii ya kubatiza na kumleta binti yangu mbele ya miguu ya Bwana,” alisema Luis Alonso Jiménez, mzee wa kanisa kutoka Kanisa Kuu la Waadventista Wasabato katika Wilaya ya Honduras ya Konferensi ya Upper Chiapas.

Uziel Roblero, mzee wa kanisa aliyewekewa mikono kutoka Konferensi ya Chiapas ya Kati, alisema alihisi furaha ya kubatiza dada yake mkubwa, Emma Roblero.
“Ni mara yangu ya kwanza kubatiza, na ilikuwa uzoefu maalum sana,” alisema. “Namshukuru Mungu kwa ajili yake na fursa ya kushiriki katika sherehe hii maalum ya ubatizo.” Emma alishiriki kwamba alihisi kubarikiwa na furaha kwa kubatizwa na kaka yake mdogo na kwa “kupeana maisha yake kwa Mungu.”
Kila mzee wa kanisa aliyepewa mafunzo huko Chiapas alipokea begi maalum la mgongoni lenye Biblia, seti za masomo ya Biblia, na wazee waliowekwa wakfu walipokea joho la ubatizo.
Mamia ya wachungaji, wainjilisti, na wanafunzi wa theolojia kutoka Chuo Kikuu cha Montemorelos na Linda Vista wataongoza kampeni hizo za uinjilisti katika makanisa 3,000 ya Waadventista kote Chiapas kuanzia Aprili 19–26, kabla ya maelfu ya ubatizo yatakayofanyika Aprili 26, 2025.
Makala asili ilichapishwa kwenye tovuti ya habari ya Divisheni ya Baina ya Amerika.